Monday, December 10, 2012

Jackline Wolper Amtambulisha Mchumba Wake Mpya Baada ya Kushindwana na Dallas




ALHAMISI iliyopita (Desemba 6, 2012), ilikuwa ni siku ya kuzaliwa ya Jacqueline Wolper, jioni yake ndani ya Synergy Lounge, Oysterbay, Dar es Salaam, alifanya bonge la pati, akiwaalika ndugu, jamaa, marafiki na majirani.

Mbele ya kila aliyehudhuria, Wolper alimtambulisha mchumba wake mpya ambaye amempiga bao, Abdallah  mtoro, ‘Dallas’ lakini akawaacha waalikwa na maswali lukuki pale alipogoma kumtaja jina.

Hakuishia hapo, akaomba mchumba wake huyo asipigwe picha hata ya kwenye simu, akisisitiza kuwa wana maana kubwa kuzuia hilo.


Mara nyingi mwenye fedha hata kama hasemi, vitendo vyake huongea, na kelele za jamaa huyo zilisomeka kwa herufi kubwa pale ulipowadia muda wa kumtuza ‘mtoto aliyezaliwa’ ambapo alimtuza cheni zenye thamani kubwa.

Wale waliomwakilisha jamaa huyo, hawakusema bei iliyonunuliwa, badala yake mmoja wao alitamka: “Cheni hizi zina thamani kubwa, kuliko zawadi yoyote ambayo inaweza kutolewa hapa.”

Cheni hizo ni mbili, moja ya shingoni na nyingine mkononi.


Mastaa kibao walihudhuria sherehe hiyo, kila mmoja alishangweka vya kutosha, huku misosi ikiwa siyo ya kuuliza, keki ilikatwa na kuliwa, shampeni zilifunguliwa na matukio mengine mengi ya kuvutia.

MC wa shughuli hiyo, Salum Mchoma ‘Chiki’, aliichangamsha sherehe na uwepo wa staa wa vichekesho, Steven Mengere ‘Steve Nyerere’, ulisababisha mbavu za waalikwa ziteseke.

Wolper, alipomtangaza mchumba wake huyo, alizungumza kwa kujiamini na madaha ndani yake na kusababisha wegeni wengi washangilie, huku wachache wakipigwa na butwaa.

Mmoja wa mastaa waliopigwa na butwaa, alihojiwa na ripota wetu na akajibu: “Kiukweli nilishangaa, unajua maneno yaliyokuwepo ni kwamba baada ya kuachana na Dallas angefulia lakini leo imekuwa tofauti ndiyo maana nimeshtuka kidogo.”

Staa huyo , alipoona atatafsiriwa vibaya, akaongeza kama aliyekumbuka kitu: “Lakini naomba ieleweke mshtuko wangu ni wa heri. Nampenda Wolper na namtakia maisha mema na huyo mchumba wake.”


Wapambe waliokuwa na mchumba huyo wa Wolper, walizungumza kwa kishindo ukumbini: “Kama kuna mtu alikuwa na mategemeo kwamba huyu mrembo atapata shida, hayo mawazo aondoe kabisa.

“Tunajua kila kitu kwamba Wolper alikuwa na mtu ambaye alishindwa kumgharamia, kwa hiyo hapa kafika. Tutamhudumia vizuri sana.”

 Kwa mjibu wa Wolper, sherehe hiyo imegharimu shilingi 19,600,000.

“Nawashukuru sana marafiki zangu waliokuja kunisapoti kwenye sherehe hii maana nimejisikia faraja ambayo sikutegemea kuipata kwa leo.

“Nimetumia milioni 19 na laki 6 kwa ajili ya kuandaa sherehe hii ili niwaburudishe marafiki  na ndugu zangu, ingawa kwa haraka haraka wengi ukiwatajia fedha hii wataona ni nyingi ila waliyokuwemo ukumbini wenyewe wataamini maana vinywaji na vyakula vyote vilikuwa vikitoka humo humo na hatukununua nje.”

CREDIT: GPL

No comments:

Post a Comment